ITAMBUE ZAWIYATUL QADIRIA

MAMBO YA WAJIBU KATIKA SWALA
Mambo ya wajibu katika swala ni kumi na moja (11). Lazima mwenye kuswali ahakikishe mambo hayo kumi na moja ameyatenda kama inavyotakiwa. Katika mambo haya kumi na moja (11) ya wajibu kuna matano (5) ni RUKNI (Yaani: Ni nguzo za Swala) na mengine sita (6) yaliyobaki si RUKNI katika swala.
Na inaposemwa “RUKNI ZA SWALA”, humaanishwa NGUZO ZA SWALA, kwa maana kwamba: Swala imesimama katika nguzo hizo tano, ikitokea nguzo moja ikaharibika au isitendeke kama inavyotakiwa au ikasahaulika katika swala basi swala itakuwa si sahihi, mwenye kuswali atatakiwa kurudia swala yake.
Ama yale mambo sita (6) ambayo sio nguzo za swala, ikitokea moja wapo kati ya hayo (sita) ikasahaulika ktk swala au kutendeka isivyotakiwa basi swala haitaharibika au tuseme: Haitakuwa batili, bali itakuwa ni swala sahihi, maana kukosea au kusahau katika hayo mambo sita ambayo si nguzo ktk swala hakuharibu swala wala kuibatilisha, isipokuwa makosa hayo au kusahau huko kukitokea ktk moja wapo ya nguzo za swala ambazo tutazitaja hivi punde.